Mbunge wa Kigoma Kaskazini -Zitto Kabwe
--
MCHANGO WA MAANDISHI WA NDG. KABWE ZUBERI ZITTO, MB KUHUSU BAJETI YA SERIKALI YA MWAKA WA FEDHA 2014/2015
Mheshimiwa
Spika, Kwanza kabisa napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa nguvu
za kuweza kuandika mchango wangu huu mdogo kwenye mjadala wa Bajeti ya
Serikali mwaka 2014/15. Kama wengi mnavyofahamu mnamo tarehe 1 Juni
mwaka 2014 nilimpoteza mama yangu mzazi na kumsitiri siku iliyofuata
tarehe 2 Juni, 2014.
Huu ni msiba mkubwa sana kwangu na ndugu zangu wote
kwani mama yetu Bi. Shida Salum alikuwa nguzo katika familia. Nafahamu
kuwa jamaa na marafiki wa mama pia wamepoteza mtu wao muhimu sana.
Napenda kuwashukuru nyote kabisa kwa salamu zenu za pole kwetu. Sina
namna ya kuelezea shukrani zangu kwenu kwani Bi Shida kwangu alikuwa
zaidi ya mama mzazi, alikuwa rafiki, dada na nguzo. Ninamshukuru Allah
kwa kuniwezesha kumwuguza na kumsitiri mama yangu. Hakuna amali kubwa
ambayo Mungu amenipa zaidi ya hiyo. Nawashukuru tena nyote kabisa
wabunge wenzangu kwa kushirikiana nami kwa namna zozote zile kumwuguza
na kumsitiri mama yangu. Mungu atawalipa malipo yanayowastahili kwa
amali na vitendo vyenu. Sisi kama familia tutaendelea kumwombea dua mama
yetu na kumtolea sadaka ili ahifadhiwe mahala pema.
Mheshimiwa
Spika, ningependa niwe nanyi katika mjadala huu muhimu wa kila mwaka wa
Taifa letu. Hata hivyo bado Mungu hajaniwezesha nguvu za kusimama na
kuzungumza. Pindi nitakapowezeshwa nguvu hizo nitakuwa nanyi kwa kipindi
hicho nitakachojaaliwa ili kushiriki katika kazi za kuendeleza Taifa
letu.
Mheshimiwa
Spika, nachukua fursa hii kumpongeza Waziri wa Fedha ndugu Saada Salum
kwa kuwasilisha Bajeti yake ya kwanza kabisa kama Waziri wa Fedha wa
pili Mwanamke wa nchi yetu. Nampongeza kwa kuchukua hatua kadhaa za
kuboresha usimamizi wa fedha za umma na hasa matamko aliyotangaza ya
kupambana na misamaha ya kodi ambayo imeongezeka mpaka kufikia asiliamia
3.5 ya Pato la Taifa na asilimia 10 ya Bajeti ya Serikali. Misamaha ya
Kodi mwaka 2012/13 ilifikia tshs 1.5 trilioni ambayo ni sawa na asilimia
15 ya makusanyo yote ya ndani na ni sawa na takribani fedha zote za
kodi ambazo Serikali ilikusanya kama kodi ya mishahara ya Wafanyakazi
(PAYE). Hata hivyo, matamko ya Serikali yana mapungufu makubwa sana na
ni matamko yale yale yanayorudiwa kila mwaka bila utekelezaji. Kuweka
wazi misamaha ya kodi na watu au asasi zilizofaidika na misamaha hiyo ni
hatua nzuri lakini haitoshi kama hatua hiyo haitaendana na kufanya
ukaguzi wa misamaha hiyo.
Kamati ya Bunge ya PAC ilitoa agizo mwaka 2013
la kutaka Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kukagua
misamaha ya kodi kama matumizi mengine yeyote ya Serikali. Ieleweke
kwamba misamaha ya kodi ni ruzuku (subsidy), ni fedha ya Serikali ambayo
iwapo ingekusanywa ingekaguliwa kwa mujibu wa sheria. Matamko ya
Serikali ya kuweka wazi misamaha lazima yaendane na kuifanyia ukaguzi
(auditing) na kuweka wazi matokeo ya ukaguzi huo. Vilevile ni lazima
sasa katika Sheria ya Fedha ya mwaka 2014/15 kuweka kipengele cha kuzuia
misamaha ya kodi kuzidi asilimia moja ya Pato la Taifa na kurekebisha
Sheria ya Ukaguzi ya umma wa mwaka 2008 ili kumpa mamlaka ya kisheria
CAG kukagua misamaha ya kodi na kuweka wazi matokeo ya ukaguzi huo kwa
umma.
Kodi kwa Wafanyakazi
Mheshimiwa
Spika, Waziri wa Fedha ametangaza nafuu ya kodi kwa wafanyakazi wa kima
cha chini kutoka kiwango cha 13% mpaka 12%. Kiwango hiki ni kidogo mno
na hakimsaidia mfanyakazi kubakia na fedha kwa ajili ya matumizi yake na
pia kwa ajili ya kujiwekea akiba. Ni dhahiri kuwa PAYE ni chanzo
kikubwa sana cha mapato ya ndani ya Serikali. Kwa mfano mwaka 2013/14
Serikali ilitarajiwa kukusanya tshs 1.5 trilioni kama PAYE ambapo tshs 1
trilioni kutoka idara ya walipa kodi wakubwa na tshs 500 bilioni kutoka
idara ya kodi za ndani. Hata hivyo, utaona kuwa mapato haya ni sawa
sawa na kodi inayosamehewa kupitia misamaha ya kodi hivyo iwapo misamaha
ya kodi ikipunguzwa mpaka kiasi cha asilimia 1 ya Pato la Taifa,
Serikali itakusanya kodi ya kutosha kuzipa pengo la punguzo la kodi kwa
wafanya kazi. Vile vile Serikali inapoteza kodi nyingi sana kupitia
ukwepaji kodi unaofanywa na makampuni makubwa ya kimataifa yanayowekeza
hapa nchini (tax evasion and tax avoidance) kwa kiwango cha asilimia 5
ya Pato la Taifa.
Iwapo Serikali itajiunga na mikataba ya kimataifa ya
kupambana na ukwepaji kodi na pia kuimarisha kitengo cha kodi za
Kimataifa ili kupambana na Multinational Corporations ambao wanatumia
njia mbalimbali kuhamisha faida zao nje, kutangaza hasara hapa nchini na
kukwepa kodi za thamani ya zaidi ya shilingi trilioni mbili kila mwaka
kwa mujibu wa takwimu za Global Financial Integrity. Napendekeza kuwa
kiwango cha chini cha kipato (mshahara) kukatwa kodi kiwe shilingi
330,000 na kiwango cha chini cha kodi kiwe asilimia 9 tu.
Mheshimiwa
Spika, Kiwango hiki cha kodi pia kinawezekana kwa Serikali kuchukua
hatua dhidi ya matumizi mabovu ya Serikali. Kwa mfano, kwa mujibu wa
Taarifa ya Mkaguzi Mkuu wa ndani wa Serikali mwaka 2013, mfumo wa
kukagua utumishi wa umma umegundua kuwa jumla ya wafanya kazi wa
Serikali 6500 walikuwa wameajiriwa mara mbili kwa majina yale yale, 2700
mara tatu na kulikuwa na watumishi 2500 waliokuwa wanachukua mishahara
miwli mpaka mitatu kila mwezi. Baada ya mfumo wa Lawson kuanzishwa jumla
ya wafanyakazi hewa 14,000 waligundulika katika jumla ya wafanyakazi
478,000 wa Serikali. Hatua ya kuondoa matumizi mabovu kutokana na kulipa
mishahara hewa pia inaweza kusaidia kupunguza mzigo wa kodi kwa
wafanyakazi nchini.
Serikali hutumia wastani wa shilingi bilioni 360
kila mwezi kulipa mishahara ambapo katika hizo shilingi bilioni Kumi
kila mwezi zimekuwa zikilipwa kwa watumishi hewa. Nafuu ya kodi kwa
wafanyakazi nchini katika sekta zote na hasa wafanyakazi wa kima cha
chini kitachochea matumizi binafsi ya bidhaa na huduma na hivyo
kuchangamsha uchumi na kuwezesha uwekaji wa akiba nchini. Nashauri
ukaguzi zaidi ufanyike katika utumishi wa umma ili kumaliza kabisa
tatizo la wafanyakazi hewa nchini.
Mheshimiwa
Spika ninapongeza kuanzishwa kwa kodi ya zuio kwa ada kwa Wakurugenzi
wa makampuni na Mashirika. Kodi hii itaongeza mapato ya Serikali. Hata
hivyo kodi kama hii pia itozwe kwenye posho ambazo viongozi wa kisiasa
na watumishi wa Serikali wanalipwa isipokuwa posho ya kujikimu (per
diem). Vile vile uamuzi wa kuagiza Wizara, Idara na Wakala za Serikali
kukusanya maduhuli kwa kutumia mashine za kielektroniki ni uamuzi muhimu
sana ambao utaongeza ufanisi katika ukusanyaji wa mapato yasiyo ya
kodi.
Kamati ya PAC iliagiza jambo hili tangu mwaka 2013 na ninaamini
kuwa Polisi wa Usalama barabarani wataanza kutoa ‘traffic notifications’
kwa njia hii; pia Wizara ya Ardhi wataanza kutoa Hati za Ardhi za
kielektroniki na kukusanya maduhuli kwa njia hii ikiwemo Wizara ya
Nishati na Madini kwa tozo mbalimbali wanazotoza. Juhudi zote hizi
lazima zionekane kwa kupunguza mzigo wa kodi kwa Wafanyakazi ambao
kiukweli ni wachache (takribani 1.3 milioni) lakini wanabebeshwa mzigo
mkubwa wa kodi kuliko wawekezaji wakubwa.
Mheshimiwa
Spika, Tanzania haiwezi kuendelea kuwa nchi ambayo Serikali yake
inaendeshwa na fedha za wafanyakazi, wafanyabiashara wadogo na wahisani.
Ni lazima makampuni makubwa ya uwezekaji nchini yashiriki kuendesha
Serikali kwa kulipa kodi stahili na kuondoa kabisa misamaha ambayo haina
mahusiano yeyote na ukuaji wa ajira nchini na kuongeza thamani ya mazao
yetu ya kilimo. Vile vile ni muhimu sana kuongeza juhudi za kukuza
ajira ili kuwa na wafanyakazi wengi ambao watapelekea kuongeza mapato ya
Serikali badala ya kukamua kundi dogo lililopo hivi sasa. Nchini Kenya
kiwango cha chini cha Kodi ya Mapato kwa wafanyakazi (PAYE) ni asilimia
10 tu kwa sababu idadi ya walipaji wa kodi hii wanafikia takribani
milioni kumi wakati Tanzania ina wafanyakazi wanaolipwa mishahara ya
kila mwezi milioni 1.3 tu.
Hifadhi ya Jamii kwa Wakulima
Mheshimiwa
Spika, Taarifa ya Hali ya Uchumi wa Taifa inaonesha kuwa Tanzania ina
jumla wa mifuko mitano ya Hifadhi ya Jamii yenye wanachama 1.3 milioni
pekee. Idadi hii ya wanachama ni 6% ya nguvu kazi ya Tanzania. Hata
hivyo nguvu kazi ya nchi haipo kwenye wafanyakazi wa mishahara pekee
kwani asilimia takribani 70 ya Watanzania wanaishi vijijini na
kujihusisha na sekta ya Kilimo. Kwa kuwa mifuko ya Hifadhi ya Jamii
haijafikia wakulima maana yake Watanzania wengi sana wanaishi ya mashaka
kwa sababu hawana Bima ya Afya, hawana mafao mengine ya muda mfupi na
wala hawana pensheni. Hali hii ni lazima kuirekebisha kama tunataka
Taifa lenye maendeleo. Hifadhi ya Jamii sio suala la pensheni tu bali
pia ni suala la uwekezaji wa akiba (savings) na uwekezaji wa ndani
(investments).
Mheshimiwa
Spika, Kasi ya ukuaji uchumi na uwekezaji (Growth and investment rates)
vina mahusiano chanya.Takwimu za Penn World Tables (2002) zinaonyesha
kuwa kwa nchi 38 za Afrika Kusini mwa jangwa la Sahara wastani wa ukuaji
uchumi ulikuwa 0.6% na wastani wa uwiano wa uwekezaji na ukuaji uchumi
ulikuwa 10%. Kwa nchi 9 za Asia (9 Asian 'miracle' economies), wastani
wa ukuaji uchumi ulikuwa 4.9% na wastani wa uwiano kati ya ukuaji uchumi
na uwekezaji ulikuwa 25%. Kasi ya ukuaji wa uchumi wa Taifa lolote
duniani unahusiana moja kwa moja na utayari wa wananchi wa nchi hizo
kuweka akiba na kuwekeza vitega uchumi. Takwimu hizi zinaonyesha dhahiri
kwamba ili Afrika ipige hatua ni muhimu sana kuimarisha uwekezaji wa
ndani ambao unatokana na kiwango cha uwekaji akiba.
Mheshimiwa
Spika, ukuaji wa uchumi wa kasi na haraka hauwezekani bila ya sekta ya
fedha iliyokita mizizi. Hata hivyo, kwa mujibu wa Taarifa ya Hali ya
Umasikini nchini (PHDR 2009) mfumo wa kibenki nchini kwetu hautoi msaada
wa kutosha kwa wafanyabiashara ndogondogo na wakulima. Mikopo kwa
uwekezaji wa ndani ni midogo sana kiasi kwamba haisaidii kuongeza
uzalishaji (productivity) na kuhimiza mabadiliko makubwa ya Uchumi
(transformation of the economy). Mikopo mingi inayotolewa na mabenki ni
kwa matumizi binafsi ya watu na mikopo mikubwa ni kwa shughuli za
uchuuzi (trading) badala ya uzalishaji. Hii inathibitishwa na Taarifa ya
Hali ya Uchumi wa Taifa ya mwaka 2013 ambayo inaonyesha kuwa katika
mikopo ya thamani ya tshs 10.3 trilioni, ni asilimia 9 tu iliyokwenda
sekta ya kilimo. 11.4% viwanda na 25% ilikwenda kwa wachuuzi. Asilimia
17 ya mikopo ilikwenda kwa watu binafsi kwa ajili ya matumizi binafsi!
Kuna haja kubwa ya kufanya mabadiliko makubwa sana ya kimuundo na kisheria na kisera ili kuhakikisha kuwa uzalishaji kwenye kilimo na uongezaji thamani wa bidhaa za kilimo unapata uhakika wa fedha za mikopo. Benki sio rafiki ya Masikini. Benki sio rafiki ya mkulima mdogo hapa nchini. Lazima kubadilika kifikra na kuachana na mazoea. Ni lazima sasa kuweka vivutio kwa wakulima kuweka akiba ya muda mrefu na kuondoa mwiko wa mkulima kutokuwa na pensheni. Hifadhi ya Jamii kwa Mkulima ni suluhisho la kuongeza akiba nchini, kupanua fursa za uwekezaji wa ndani tena kwenye kuongeza uzalishaji wa Kilimo na kujenga jamii ambayo inahifadhiwa. Hifadhi ya Jamii kwa Mkulima pia itaongeza ushindani dhidi ya mabenki katika soko la mikopo midogo midogo na hivyo kumfaidisha mkulima.
Mheshimiwa
Spika, mabilioni ya fedha tunayoona yanamilikiwa na mabenki, mifuko ya
hifadhi ya jamii, kampuni za bima na asasi za uwekezaji ni matokeo ya
kukusanya viakiba vya mtu mmoja mmoja kutoka kwa mamilioni ya watu. Kazi
ya asasi za fedha ni kukusanya mabilioni haya na kuyaelekeza kwenye
uwekezaji wa miradi mikubwa ianyofanywa na wafanyabiashara na hata
miradi midogo kwa wafanyabiashara wadogo. Katika bara la Afrika, hivi
sasa watu masikini wanaweka akiba zao katika vyama vya kuweka na kukopa
(SACCOS). Hii ni hali halisi Tanzania, hali ambayo lazima tuijenge kwani
mabenki hayapendi kuendesha akiba ndogondogo za watu masikini.
Mifuko
ya Hifadhi ya Jamii imeanza mafao ya mikopo kwa SACCOS za wanachama wao
na hivyo kuweza kukopa kwa lengo la kuendesha maisha yao kwa kuongeza
uzalishaji hasa kwenye Kilimo. Wafanyakazi wa Sekta rasmi wametungiwa
sheria kwamba ni lazima sehemu ya mishahara yao wakatwe kama akiba ya
uzeeni na majanga mengine. Waajiri wao pia hukatwa fedha kuchangia
pensheni za wafanyakazi wao. Mkulima hana sheria ya kumlazimisha kuweka
akiba (na sio lazima kuwepo kwa sheria hiyo) na pia hana ‘mjomba’ wa
kumchangia sehemu ya pensheni yake. Hata hivyo Mkulima anachangia 25% ya
Uchumi wa Tanzania (GDP) na pia fedha za kigeni. Mchango wa bidhaa za
kilimo kwenye mauzo nje umekuwa mdogo kwa sababu wakulima wananyonywa na
mabenki na hawana fursa ya mikopo ya kupanua mashamba yao, kununua
pembejeo na kufikia masoko mazuri ya bidhaa zao.
Mheshimiwa
Spika, Hali ya Uchumi wa Taifa 2013 inaonesha kuwa 20% ya mapato ya
fedha za kigeni nchini yanatoka kwenye bidhaa za kilimo ambacho ni
Pamba, Kahawa, Tumbaku, Chai, Korosho, Karafuu na Katani. Mazao haya
yanaingiza jumla ya dola za kimarekani 867 milioni. Uchumi wetu hauwezi
kuondoa umasikini kwa sababu shughuli zake zimejikita kwenye sekta ya
madini ambayo inachangia ajira kiduchu (an enclave) lakini inachangia
40% ya mauzo nje. Uchumi wetu ni egemezi na tegemezi kwa sekta moja tu
jambo ambalo ni hatari sana kwa ustawi wa maisha ya wananchi.
Ni wajibu
wa Serikali kuweka mazingira ya kuongeza uzalishaji wa mazao ya Kilimo
na hivyo kuongeza mapato ya fedha za kigeni na kuondoa umasikini
vijijini. Mauzo ya bidhaa za kilimo nje yameshuka kwa kiwango cha
asilimia 9, zao la Tumbaku ambalo ndio linaongoza kwa kuingiza fedha za
kigeni dola za marekani 307 milioni (zaidi ya shilingi bilioni 500 za
kitanzania), mauzo yake yaliporomoka kwa kiwango cha asilimia 12
kutokana na wakulima kutotumia mbolea kwa sababu ya kukosa mikopo katika
mabenki kulikosababishwa na unyonyaji wa zaidi ya shilingi bilioni 28
kwa mujibu wa taarifa ya ukaguzi. Mauzo ya Pamba yalishuka kwa asilimia
32 kutokana na mgogoro wa bei uliosababishwa na kutokuwepo kwa sera ya
kufidia bei kwa wakulima (price stabilisation).
Mheshimiwa
Spika, suluhisho la mambo yote haya ni kuingiza wakulima kwenye hifadhi
ya jamii ili waweke akiba, wapate mafao ya muda mfupi na mrefu na
wapate mikopo kupitia vyama vyao vya ushirika vya kuweka na
kukopa(AMCOS). Mabenki hayataendelea tena kunyonya wakulima kwa sababu
riba zinazotolewa kwa mikopo ya SACCOS/AMCOS ni nafuu na zinaendana na
hali halisi ya wakulima. Kupitia kujiunga kwao katika Hifadhi ya Jamii,
Fao la fidia ya bei laweza kuanzishwa ili kuwafidia wakulima pale bei za
mazao yao zinaposhuka chini ya gharama zao za uzalishaji.
Mheshimiwa
Spika, katika jimbo langu la uchaguzi tumefanya mradi huu na hivi sasa
wakulima wa kahawa wa vijiji vya Matyazo, Mkabogo na Rusaba kupitia
chama chao cha Ushirika cha RUMAKO ni wanachama wa NSSF na tayari
wameanza kufaidika na mafao kama bima ya afya na mikopo yenye riba
nafuu. Kufuatia mafanikio ya RUMAKO vyama vingine vya ushirika
vinavyounda chama kikuu cha KANYOVU chenye vyama 12 vya msingi
wamejiunga na NSSF. Tunaweza kusema kwa uhakika kabisa kuwa wakulima
wote wa kahawa wa mkoa wa Kigoma wanahifadhi ya Jamii kupitia vyama vyao
vya ushirika. Shirika la NSSF sasa limeanzisha mpango wa kuandikisha
wakulima wengi zaidi nchi nzima kupitia ‘Wakulima scheme’. Katika mpango
huu NSSF wameshirikiana na Tume ya Ushirika nchini ambayo kuanzia
january, 2014 imepewa jukumu la kudhibiti na kusimamia vyama vya
ushirika nchini. Ni hatua ya kupigiwa mfano. Hata hivyo bila vivutio vya
serikali wakulima hawatajiunga na hifadhi ya jamii kwa wingi tunaoutaka
ili kubadilisha kabisa uchumi wa watu wetu vijijini.
Mheshimiwa Spika, Napendekeza ifuatavyo
Serikali
ianzishe mpango wa kuwachangia wakulima wanaojiunga na Hifadhi ya Jamii
kwa uwiano wa theluthi ya michango yao. Kwa mfano iwapo mkulima
atachangia tshs 20,000 kwa mwezi basi Serikali imchangie tshs 10,000 kwa
mwezi kwa sharti kwamba iwapo atajitoa kwenye hifadhi ya jamii huu
mchango wa Serikali hataupata lakini iwapo akikaa kwenye hifadhi ya
jamii kwa miaka isiyopungua kumi/umri wa kustaafu ataweza kupata
michango yote na mafao stahiki kwa mujibu wa sheria kama mfanyakazi wa
sekta rasmi.
Serikali
iachane na mpango wa kuanzisha ‘price stabilisation fund’ na badala
yake iweke sera kwamba wakulima waliokwenye Hifadhi ya Jamii moja ya fao
watakaolipata ni fao la fidia ya bei ambalo litalipwa kwa namna ambayo
wataalamu wa ‘actuarial’ wataona ni endelevu.
Serikali
kupitia Msimamizi wa Hifadhi ya Jamii nchini (SSRA) waelekeze kuwa
mifuko itenge angalau 40% ya akiba wa wakulima kwenye uwekezaji wa
kuendeleza miundombinu ya kilimo, kuongeza thamani ya mazao ya kilimo na
kutoa mikopo yenye riba nafuu kwa wakulima kupitia SACCOS/AMCOS
Mheshimiwa
Spika, iwapo kwa mfano wakulima milioni moja tu nchini walio kwenye
vyama vya Ushirika wakijiunga katika hifadhi ya jamii na kuchangia
kiwango cha chini kabisa cha tshs 20,000 kwa mwezi (michango
itakayokatwa kulingana na msimu wa kilimo cha zao husika) na serikali
kuweka kivutio cha tshs 10,000 katika kila mchango wa mkulima mmoja
mmoja katika idadi hiyo, jumla ya Michango itakayokusanywa nitakuwa ni
tshs 360 bilioni. Wakulima hawa watapata bima ya afya wao, wenza wao na
wategemezi 4 na hivyo bima ya afya kufikia Watanzania milioni 6. Fedha
hizi zitatumika kuwekeza kwenye miradi ya uzalishaji katika sekta ya
kilimo ikiwemo mikopo ya pembejeo, ujenzi wa miundombinu ya kilimo na
viwanda vya kuongeza thamani ya mazao ya kilimo. Mifuko ya Hifadhi ya
Jamii inaweza kuwekeza fedha hizi kama hisa kwenye Benki ya Kilimo na
kuwezesha uwekezaji mkubwa katika sekta ya kilimo. Hii ndio inaitwa
‘Transformation’.
Mheshimiwa Spika naomba kuwasilisha
Kabwe Zuberi Zitto, Mb
Kigoma Kaskazini.
Kigoma. Juni 17, 2014.
zitto kabwe ametoa maoni mazuri ktk bajeti serikali iyafanyie kazi
ReplyDelete